Pata taarifa kuu
TOUR DE FRANCE

Mwingereza Chris Froome ndiye Bingwa wa Mashindano ya 100 ya Tour de France akichukua taji kutoka kwa Bradley Wiggins

Mashindano ya Baiskeli ya Tour De France ambayo yalikua ya mia moja tangu kuanzishwa kwake yamefikia tamati na raia wa Uingereza Chris Froome amefanikiwa kushinda mbio hizo kwa mwaka huu. Froome amefanikiwa kutwaa ubingwa huo akiwa Mwingereza wa pili kutwaa taji hilo akifuata nyayo za Bradley Wiggins aliyeibuka kinara wa mbio hizo za baiskeli za Tour de France mwaka jana.

Mshindano wa Mashindano ya Baiskeli ya Tour de France Chris Froome akionesha maua baada ya kutangazwa mshindi
Mshindano wa Mashindano ya Baiskeli ya Tour de France Chris Froome akionesha maua baada ya kutangazwa mshindi
Matangazo ya kibiashara

Kijana huyo kabla ya kuibuka mshindi wa jumla wa mashindano ya baiskeli ya Tour de France aliibuka kinara kwenye hatua hatua nyingine za awali hasa ile ya nane, kumi na tano na kumi na sana.

Froome pia licha ya kuibuka mshindi wa Tour de France mwaka huu huko nchini Ufaransa alikutana na vikwazo kadhaa ikiwa ni pamoja na kulimwa faini mara mbili kwenye mashindano ya hatua ya kumi na nane kutokana na kula chakula kinyume na ilivyopangwa.

Raia huyo wa Uingereza amefanikiwa kuongoza kwa kuendesha baiskeli yake kwa umbali wa kilometa 3,404 na kufanikiwa kutwaa jezi ya njano na kuibuka na donge nono la pauni laki tatu na elfu themanini ambazo watagawana na wenzake.

Froome baada ya kuibuka na ushindi huo amekiri mafanikio yake yametokana na ushirikiano aliokuwa anaupata na timu yake licha ya kwamba alikuwa anakabiliwa na vikwazo kadhaa.

Mshindo wa Tour de France mwaka jana Wiggins aliamua kuchukua hatua ya kutoshiriki kwenye kinyang'anyiro hicho kutokana na kukabiliwa na tatizo la majeraha na sasa huenda akashiriki mwakani.

Meneja wa Timu ya Sky anakotoka Froome, Sir Dave Brailsford amekiri hayo ni mafanikio ambayo wanapaswa kujivunia baada ya kushuhudiwa wakiubuka vinara kwenye mashindano hayo makubwa ya baiskeli duniani.

Changamoto pekee ambayo ipo mbele ya Froome ni kuhakikisha anajiepusha na utumiaji wa dawa za kusisimua misuli kama alivyofanya bingwa mara saba Lance Armstrong aliyekiri hakuna anayeweza kushinda mashindano hayo mara nyingi kama hatumii dawa hizo.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.