UN yasitisha misafara ya misaada nchini Syria baada ya kushambuliwa, Urusi yalaumiwa
Umoja wa mataifa umesimamisha misafara yake yote ya misaada nchini Syria, saa chache baada ya shambulizi la anga lililolenga msafara wake, tukio ambalo inasema ni uhalifu wa kivita.
Imechapishwa:
Uamuzi huu wa umoja wa Mataifa kusitisha kupelekwa kwa misaada kwenye mji huo, umekuja saa chache baada ya magari yake 18 yaliyokuwa yamebeba misaada ya kibinadamu, kushambuliwa magharibi mwa Aleppo, ambapo watu 12 wameripotiwa kufa.
Umoja wa Mataifa inasema kuwa, uamuzik huu umechukuliwa kama hatua za awali za kiusalama dhidi ya wafanyakazi wake na magari yanayotumiwa kufikisha misaada hiyo kwenye maeneo yaliyoathirika, na kwamba wanafanya tathmini zaidi kabla ya kuamua hatua zaidi za kuchukua.
Afisa wa umoja wa Mataifa amewaambia wanahabari kuwa, misaada hiyo ilikuwa ikiingia kwenye mji wa Aleppo baada ya kupata kibali kutoka kwa Serikali kufika kwenye maeneo ya mjik huo ambayo yameathirika kwa vita.
Marekani inasema mpaka sasa haijafahamika ikiwa nik ndege za Urusi ama zile za Serikali ya Syria ndizo zilizotekeleza shambulio dhidi ya magari takribani 31 ya umoja wa Mataifa, huku taarifa za hivi punde zikiuoneshea kidole utawala wa Moscow ambao ni mshirika wa karibu wa Serikali ya Syria.
Kufuatia shambulio hili, umoja wa Mataifa sasa umetangaza kusitisha kupelekwa kwa misaada nchini Syria, huku waangalizi wa haki za binadamu wakisema kuwa shambulio hili litaathiri shughuli za mashirika ya misaada ambayo yamekuwa yakifanya kazi kwenye maeneo yenye vita.