WHO yaishtumu Tanzania kwa kutotoa taarifa muhimu kuhusu Ebola
Shirika la afya duniani WHO limeishtumu serikali ya Tanzania kwa kushindwa kutoa taarifa za wasiwasi wa kuwepo kwa maambukizi ya Ebola nchini humo, suala ambalo linarudisha nyuma vita dhidi ya ugonjwa huo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
WHO katika taarifa yake imesema ilipata taarifa kuwa, tarehe 10 mwezi Septemba kesi ya Ebola iliripotiwa katika jijini la Dar es salaam baada ya mgonjwa aliyekuwa anashukiwa kugundulika kuambukizwa.
Licha ya kuomba taarifa rasmi, WHO inasema haijapata majibu yoyote kutoka kwa serikali ya Tanzania kuhusu madai ya kuwepo kwa maambukizi hayo.
Hata hivyo, serikali ya Tanzania kupitia Wizara ya afya siku kadhaa zilizopita, ilikanusha kuwepo kwa Ebola nchini humo lakini ikatoa tahadhari kwa raia wake kuwa makini.
Taarifa hii ya WHO imekuja, wakati huu mataifa ya Afrika Mashariki yakiwa katika hali ya tahadhari kutokana na maambukizi ya Ebola Mashariki mwa Jamhuri ya Kidmekrasia ya Congo, ambako watu 2,103 wamepoteza maisha kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
Nchini Uganda, watu wanne waliripotiwa kuambukizwa wote waliokuwa wamevuka mpaka kutoka DRC lakini baadaye wakapoteza maisha.