Utafiti: Watu waliopona virusi vya Ebola wasumbuliwa na figo
Utafiti wa watalaam wa afya uliofanywa nchini Guinea unaonesha kuwa, watu wengi walipona baada ya kupata chanjo ya Ebola, afya yao ilidhoofika baada ya kuanza kusumbuliwa na figo.
Imechapishwa:
Watafiti katika ripoti yao iliyochapishwa katika Jarida la afya la Lancet, wamesema wamethibitisha hilo baada ya kuwafanyia uchunguzi watu 1,100 waliponea wakati wa mlipuko wa ugonjwa huo katika nchi za Afrika Magharibi miaka miwili iliyopita.
Aidha, ripoti inaeleza kuwa watu 59 walifariki dunia, mwaka mmoja baada ya kupewa chanjo na tiba ya Ebola, na asilimia 62 ya vifo vyote vimeelezwa ni kutokana na kuathiriwa kwa figo zao.
Kinachoshangaza ni kuwa, idadi kubwa ya watu wanaopoteza maisha, ni wale waliokaa hospitalini muda mrefu.
Watalaam wa afya wanasema, uchunguzi wa kina unastahili kufanywa ili kubaini ni kwanini watu hao waliokuwa wamepata matibabu na kuaminiwa kupona, walikuwa wanafariki dunia kutokana na matatizo ya figo.
Ripoti hii imekuja, wakati huu Ebola ikiendelea kuzua wasiwasi Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambako kwa kipindi cha mwaka mmoja, watu zaidi ya 2,000 wamepoteza maisha na zaidi ya 3,000 kuambukizwa virusi vya ugonjwa huo hatari.