Serikali ya Kenya yasema hakuna Ebola nchini humo
Serikali ya Kenya imewahakikishia raia wa nchi hiyo na wageni kuwa hakuna maambukizi yoyote ya Ebola yaliyoripotiwa nchini humo.
Imechapishwa:
Hii ni baada ya mwanamke mmoja kulazwa katika Kaunti ya Kericho, baada ya kushukiwa kuwa alikuwa na dalili za Ebola.
Mwanamke huyo alikuwa amesafiri kutoka Malaba katika eneo la mpaka na Uganda, baada ya virusi hivyo kuripotiwa Magharibi mwa nchi hiyo.
Waziri wa afya nchini humo Sicily Kariuki amesema kuwa baada ya uchunguzi dhidi ya mwanamke huyo mwenye umri wa miaka 36, imebainika kuwa hakuwa na Ebola.
Hata hivyo, Waziri huyo amesema kuwa mgonjwa huo alikuwa na dalili kama za mgonjwa wa Ebola ambazo ni pamoja na kuumwa kwa kichwa, homa kali na kutapika.
'Watalaam wetu wamemfanyia uchunguzi mgonjwa huyo na imebainika kuwa hakuwa na Ebola, kwa sasa anaendelea vizuri,” alisema.
“Nawahakikishia Wakenya wote na wageni kuwa hatuna hatuna hata kisa kimoja cha Ebola,” ameongeza.
Kenya imechukua tahadhari katka mpaka wake wa Busia na Malaba kuhakiksiha kuwa watu wote wanapimwa kuhakikisha kuwa hawana Ebola.
Ugonjwa wa Ebola, umeendelea kusababisha maafa Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambapo kuanzia mwezi Agosti mwaka 2018, watu 1,400 wamefariki dunia na wengine zaidi ya 2,000 wakiambukizwa.
Kenya haijawahi kuripoti kisa hata kimoja cha Ebola.