Uganda kuanza kutoa chanjo ya Ebola
Wizara ya afya nchini Uganda inatarajiwa kuanza kutoa chanjo ya kuzuia maambukizi ya ugonjwa hatari wa Ebola nchini humo licha ya kutoripotiwa kwa maambukizi yoyote.
Imechapishwa:
Chanjo hiyo itaanza kutolewa kwa wafanyikazi wa afya, kuanzia siku ya Jumatatu, kama tahadhari kwa sababu ya kuendelea kusambaa kwa ugonjwa huo Mashariki mwa DRC, katika Wilaya ya Beni inayopakana na Uganda.
Uganda ambayo imewahi kusumbuliwa na maambukizi haya katika siku zilizopita, inakuwa nchi ya kwanza duniani, kutoa chanjo hii bila ya kuwepo kwa maambukizi ya Ebola.
Takwimu za Wizara ya afya nchini DRC na Shirika la afya duniani, zinaonesha kuwa watu 182 wamepoteza maisha Mashariki mwa DRC, kutokana na maambukizi ya Ebola.
Watu wengine 258 wameambukizwa katika jimbo hilo la Kivu Kaskazini.