Kampeni za kuifanyia mabadiliko katiba ya Burundi zaanza rasmi
Kampeni za kuibadilisha Katiba ya Burundi kupitia kura ya maoni ziliaza rasmi hapo jana, licha ya Umoja wa Mataifa na Umoja wa Ulaya kuionya serikali ya Burundi kuhusu mabadiliko hayo ya katiba.
Imechapishwa:
Raia wa nchi hiyo, wanatarajiwa kupiga kura tarehe 17 mwezi huu kuibadilisha Katiba, mabadiliko ambayo yatamwezesha rais Pierre Nkurunziza kuendelea kusalia madarakani kwa miaka 16 zaidi.
Wanasiasa wa upinzani wanaoishi nje ya nchi hiyo chini ya muungano wa CNARED wamewataka raia wa Burundi kupinga mabadiliko hayo.
Nchini Burundi imekuwa ni vigumu kwa wapinzani kujitokeza waziwazi na kupinga mabadiliko hayo kwa hofu ya kukamatwa na kufungwa jela.
Raia wa nchi hiyo wanasema wana hofu ya kutokea machafuko kufuatia mabadiliko hayo ya katiba.
Makundi mbalimbali ya watu kutoka ndani na nje ya chama tawala cha CNDD-FDD yamekua yakipinga katiba kufanyiwa mabadiliko, wakimshtumu rais Nkurunziza kutaka kuitumbukiza tena Burundi katika dimbwi la machafuko.