Wafungwa mia saba wakiwemo wa kisiasa waachiwa huru Burundi
Takribani wafungwa mia saba arobaini,wengi wao walioshiriki maandamano ya kumpinga raisi Pierre Nkurunziza mnamo mwaka 2015 wameachiwa huru jana ijumaa nchini Burundi serikali imetangaza.
Imechapishwa:
Wafungwa hao waliachiwa huru kutoka katika gereza kubwa zaidi la Mpimba jijini Bujumbura chini ya muongozo wa waziri wa sheria Aimee-Laurentine Kanyana, tukio lililoshuhudiwa na baadhi ya mabalozi wa mataifa ya magharibi.
Kuachiliwa kwao huru kunakuja baada ya msamaha wa raisi mwishoni mwa mwaka jana.
Wafungwa 450 kati ya 740 walishiriki katika harakati za uasi mwaka 2015 kumpinga raisi aliyeko madarakani alieleza waziri Kanyana.
Balozi mmoja aliiambia AFP kwa sharti la kutotaja jina kuwa ni hatua nzuri iliyofikiwa na ofisi yake itatoa taarifa baada ya kuzingatia taratibu za kiofisi.
Hata hivyo waziri wa sheria nchini Burundi Aimee-Laurentine Kanyana amewaonya wafungwa hao walioachiwa huru kutorejea kutenda makosa hayo kwani adhabu yake ni kifungo cha maisha.