Marekani yapongeza hatua ya Kenyatta na Odinga kumaliza tofauti za kisiasa
Marekani imepongeza hatua ya viongozi wa kisiasa nchini Kenya, rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa upinzani Raila Odinga kukutana na kuahidi kuanza mchakato wa maridhiano ya kisiasa.
Imechapishwa:
Waziri wa Mambo ya nje wa Marekani Rex Tillerson ambaye amezuru nchi hiyo, amesema viongozi hao wawili, wamefanya maamuzi ambayo yatasaidia kuimarisha umoja wa taifa hilo ambalo limegawanyika kisiasa.
Kenyatta na Odinga walikutana jana kwa mara ya kwanza tangu kumalizika kwa Uchaguzi tata mwaka 2017.
Wawili hao wamekubalian kuzika tofauti zao za kisiasa kwa maslahi ya nchi hiyo ya Afrika Mashariki. Imekubaliwa kuwa Tume maalum kuundwa ili kushughulikia mambo yote yanayoligawa taifa hilo kwa misingi ya kisiasa na kikabila.
Hatua hii haikutarajiwa na wandani wa wanasiasa hao wawili.
Moses Wetangula, mmoja wa viongozi wenza katika muungano NASA amesema walisikia kuhusu mkutano huo kupitia vyombo vya Habari na sasa watakutana na Odinga siku ya Jumatatu wiki ijayo kufahamu kwa undani kilichojiri.
Wachambuzi wa siasa nchini Kenya licha ya kupongeza kukutana kwa viongozi hao, imekuwa ni vigumu kufahamu kuhusu nini hasa kilichowasukuma Odinga na Kenyatta kukutana baada ya misimamo mikali.