Raia wa Burundi waendelea kuikimbia nchi yao
Madaktari wasiokuwa na mipaka wanasema, wakimbizi kutoka Burundi wanaoishi Tanzania wanakabiliwa na hatari ya kiafya kutokana na ongezeko kubwa la wakimbizi wanaoendelea kuingia nchini humo.
Imechapishwa:
Wakimbizi hao wanapewa hifadhi katika kambi za Nyarugusu, Mtendeli na Nduta Magharibi mwa Tanzania.
Madaktari hao wanasema kuwa kambi ya Nduta ambayo kwa sasa inawahifadhi wakimbizi 117,000 inatarajiwa kuwapa hifadhi wakimbizi zaidi ya 150,000 kufikia mwezi Aprili.
Raia wa Burundi wanaendelea kuikimbia nchi yao kutokana na hali ya usalama kuendelea kuzorota, licha ya serikali kutangaza kwamba hali ya usalama ni shwari.
Zaidi ya watu 300,000 wameyahama makaazi yao, na kukimbilia nje ya nchi kutokana na mauaji na visa vya kukamatwa kiholela ambavyo vinaendelea kushuhudiwa nchini Burundi, kwa mujibu wa mashirika ya kimataifa ya haki za binadam.