UN yasema wakimbizi bandia 42,000 wamekuwa wakiishi Daadab
Umoja wa Mataifa unasema Wakenya 42,000 wamekuwa wakiigiza kuwa ni wakimbizi kutoka nchini Somalia na kuishi katika kambi ya Daadab Kaskazini mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Umoja huo sasa umesema wakimbizi hao bandia wataondolewa katika kambi hiyo na kupelekwa eneo lingine katika jitihada za kupunguza idadi ya wakimbizi katika kambi hiyo kutoka 343,000 hadi 193,000 kufikia mwisho wa mwaka huu.
Msemaji wa Shirika la wakimbizi la UNCHR nchini Kenya Duke Mwancha ameliambia Gazeti la Daily Nation kuwa, wakenya hao wamekuwa wakijisajili kama wakimbizi ili kupata mahitaji muhimu kama chakula.
Serikali ya Kenya mwezi Mei mwaka huu ilitangaza kuwa itafunga kambi hiyo ya wakimbizi na kuwarejesha nyumbani kwa sababu za kiusalama.
Umoja wa Mataifa unasema unahitaji Dola za Marekani Milioni 115.4 kufanikisha juhudi za kuwarudisha nyumbani wakimbizi hao na kufunga kambi hiyo.