Somalia: Kuifunga kambi ya Daadab ni kukaribisha ugaidi
Waziri mkuu wa Somalia, amesema kuifunga kambi ya wakimbizi ya Daadab iliyoko nchini Kenya, itawawia vigumu sana kwa upande wao, huku akishauri muda wa mwisho wa kufungwa kwa kambi hiyo iwe mwaka 2019.
Imechapishwa:
Waziri mkuu, Omar Abdirashid Ali Sharmarke, amekiambia kituo kimoja cha Marekani kuwa "tunataka wakimbizi wa nchi yetu warudi nyumbani moja kwa moja, lakini ni muhimu kuwa na mpango wa namna watakavyorejea. hauwezi tu kuwafurusha bila ya kuwa na kitu." alisema waziri mkuu Sharmarke.
Waziri mkuu huyo ameongeza kuwa Serikali yao bado inaendelea na mazungumzo na Serikali ya Kenya, kuangalia uwezekano wa kuongezwa kwa muda zaidi wa kuifunga kambi hiyo, na kwamba muda wa miaka mitatu ndio unafaa zaidi kwa sasa.
Sharmarke amesema kuwa "hawataki Serikali ya Kenya ilazimishe wakimbizi kurudi nyumbani wakati huu, kwasababu kutatengeneza hali tete zaidi ya usalama ikiwa watafurushwa tu, ikiwa hakuna miundombinu muhimu wanakorejea. Wengi ni vijana na wakilazimishwa kurudi huenda wakajiunga na makundi ya kiislamu." alisema waziri mkuu.
Utawala wa Mogadishu unaona kuwa uamuzi wa Serikali ya Kenya kutaka kuifunga kambi hiyo, umezingatiwa kisiasa zaidi kuliko uhalisia wa mambo.
Serikali ya Somalia pia imekanusha vikali kuwa shambulio lililotekelezwa kulenga chuo kikuu cha Garissa, mpango wake ulipangwa kwenye kambi ya Daadab.
Kauli ya waziri mkuu Sharmarke inakuja ikiwa ni siku moja tu imepita toka umoja wa Mataifa uunge mkono hatua ya Kenya kutaka kuifunga kambi ya Daadab, hatua ambayo inakosolewa vikali na mashirika ya misaada.