Malaria bado ni changamoto pwani ya Kenya
NAIROBI – Dunia mnamo Aprili 25 inaadhimisha siku ya kimataifa ya Malaria, ambapo mipango mbalimbali inafanyika katika jitihada za kukabiliana na maradhi hayo.Mwandishi wa RFI Kiswahili Diana Wanyonyi, anaripoti akiwa pwani ya Kenya.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Nchini Kenya, katika jimbo la Kilifi mkoani Pwani, kuna mama mmoja aliyejitokeza kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kutumia vyandarua kujikinga na mbu wanaosababisha Malaria.
Mwanajuma Athman, anajulikana sana na wanakijiji kama mama neti, hii ni baada ya kuwa mstari wa mbele kupiga vita ugonjwa wa malaria kwa kuhakikisha kila mtu analala ndani ya neti licha ya baadhi ya watu katika jamii kupinga masuala ya neti.
Tukapata kwamba neti zilikuwa kidogo huko kwa jamii, mzungu tulipomrudishia majibu, alikubali kuleta neti kwa kijiji. Swali lilikuwa ni mbona hatujapata mtu sahihi aliyesema kwamba neti ni mbaya. Amesema Mwanajuma Athman.Mwanajuma Athman, mama neti
Mwandishi Diana, pia alipata fursa ya kuzungumza na Selina Ndunthi, mama ambaye mwanawe alifariki kutokana na ugonjwa wa Malaria.
Nilikuwa nimeenda kupanda migomba yangu mitatu, nilipomaliza kuipanda ndio nilimuona huyo msichana wangu niliyekuwa nimemwacha nyumbani akinifuata mbio, akisema mtoto ameanza na kutapika akitoa jicho hivi, nikaenda kumuita baba mdogo na wameenda hospitali, nilipofika huko mtoto alikuwa amekufa tayari. Amesema Selina.Selina Nduthi, mwanaye alikufa kutokana na Malaria
Katika kituo cha afya cha Mavueni nakutana na muuguzi mkuu Onesmus Mwaten anayesema kando na tiba, wao hutoa mafunzo kwa jamii kuhusu umuhimu wa kutumia neti ili kuepuka ugonjwa wa Malaria.
Wale ambao hawajui neti zinapatikana wapi, waweze kufika kwa zahanati wapate ushauri, wapate neti. Amesema Onesmus.Onesmus Mwathen, muuguzi mkuu Mavueni
Kando na juhudi za serikali kuu na pia asasi za kijamii, ipo haja ya raia pia kujituma na kuiga mfano wa mama neti ili kuangamiza ugonjwa wa Malaria.
Dunia ikiadhimisha siku hii, kauli mbiu ya mwaka huu ni "Wakati wa kutokomeza Malaria: wekeza, vumbua, tekeleza". Shirika la afya duniani WHO, litazingatia kipengee cha tatu ambacho ni kutekeleza, haswa umuhimu wa kufikia watu waliotengwa katika mikakati inayopatikana kwa sasa.