Rwanda yamteua Vincent Karega aliyefukuzwa Kinshasa kuwa balozi Brussels
Rwanda imemteua balozi mpya mjini Brussels. Takriban miezi mitano baada ya kufukuzwa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, balozi wa zamani wa Rwanda mjini Kinshasa Vincent Karega amepewa tena wadhifa wa kidiplomasia, safari hii nchini Ubelgiji.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu mjini Kigali, Lucie Mouillaud
Vincent Karega ataongoza taasisi kubwa ya kidiplomasia ya Rwanda katika bara la Ulaya. Akiwa ameteuliwa kutoka orodha nzima ya mabalozi wapya, tarehe ya kuchukua madaraka yake mjini Brussels bado haijabainishwa.
Akihudumu kama balozi mjini Kinshasa kuanzia mwezi Julai 2020, mwanadiplomasia huyo, mzaliwa wa mkoa wa Kivu Kaskazini nchini DRC, haraka aliona uhusiano na DRC ukizorota wakati, mwishoni mwa mwaka 2021, kundi lenye silaha la M23 lilipoanzisha mashambulizi yake mashariki mwa nchi na kuungwa mkono na Kigali kulingana na mamlaka ya Kongo, jambo ambalo Rwanda imekuwa ikikanusha.
Lakini shutuma hizi na kusonga mbele kwa waasi kwenye uwanja wa vita, viliifanya serikali ya Kinshasa kumfukuza balozi huyo mwezi Oktoba mwaka jana, na kuacha wadhifa wake wazi nchini humo. Uamuzi ambao Kigaliiliupokea wakati huo "kwa masikitiko".
Kabla ya DRC, Vincent Karega alikuwa alozi wa Rwanda kwa miaka minane mjini Pretoria. Kipindi ambacho kilidhihirika na kufukuzwa kwa wanadiplomasia mwaka 2014, mamlaka za Afrika Kusini zikiwatuhumu wajumbe wa Rwanda kuhusika katika mashambulizi katika ardhi yake dhidi ya wapinzani wa utawala wa Rais Paul Kagame. Madai ambayo yalikanushwa na Kigali.