DRC: UN yawataka waasi wa M23 kuondoka katika maeneo wanayokalia
NAIROBI – Katibu mkuu wa umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, ametoa wito kwa kundi la waasi wa M23 nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, kuheshimu makubaliano ya usitishaji mapigano na kuondoka bila masharti katika maeneo wanayoyakalia mashariki mwa nchi hiyo.
Imechapishwa:
Cheza - 01:01
Kauli ya Guterres, ameitoa wakati huu waasi hao wakiwa wanaendelea kushikilia maeneo kadhaa ya mashariki mwa DRC, tangu walipoanza tena uasi mwishoni mwa mwaka 2021.
Kwa mujibu wa msemaji wake, Stephen Dujarric, katibu mkuu amewataka wapiganaji wa M23, kuheshimu makubaliano ya usitishaji mapigano na kuondoka kwenye maeneo wanayoyashikilia ili kurejesha amani.
Aidha Guterres, amealaani vurugu na mauaji dhidi ya raia, akiyataka makundi mengine ya kigeni yanayofanya shughuli zao nchini humo, kuweka silaha chini na kuzisalimisha bila masharti.
Uasi wa kundi la M23, umesababisha kuchochea mzozo kati ya nchi ya DRC na Rwanda, ambapo Kinshasa imekuwa ikiutuhumu utawala wqa Kigali kuwasaidia waasi hao, tuhuma ambazo hata hivyo Rwanda inaendelea kukanusha.
Kauli ya Guterres, imefanana na ile iliyotolewa na rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron, ambaye akiwa ziarani jijini Kinshasa, aliyataka makundi hayo kusitisha mapigano bila hata hivyo kuikosoa Rwanda kama rais wa DRC, Felix Tshisekedi alivyokuwa akitaka.