Marekani yataka uchaguzi huru na haki nchini Kenya huku bunge likivunjwa
Marekani kupitia Waziri wake wa Mambo ya nje, Anthony Blinken inatoa wito wa kufanyika kwa uchaguzi huru na haki nchini Kenya, baada ya Tume ya Uchaguzi kutangaza majina ya wagombea wanne wanaotafuta urais, na kampeni kuanza.
Imechapishwa:
Wito huu umekuja baada ya mmoja wa wagombea wakuu, naibu rais William Ruto, kudai kuwa, kuna njama za kuiba kura.
Wakati hayo yakijiri, kura za maoni za hivi punde, kutoka Shirika la Infotrack, zinaonesha kuwa Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga anaongoza, utafiti ambao umetupiliwa mbali na Ruto.
Katika hatua nyingine, bunge limevunjwa kuelekea uchaguzi Mkuu mwezi wa nane.
Bunge la 12 limekuwa tulivu kinyume na lile la 11 ambalo lilishuhudia majibizano makali ya wabunge wa upinzani na wale wa serikali, baada ya kupitishwa kwa mswada tata kuhusu usalama.
Wabunge waliomaliza muda wao, watakumbukwa kwa kuruhusu serikali ya rais Uhuru Kenyatta kukopa kiasi kikubwa cha fedha kinyume na serikali zilizopita.
Aidha, bunge hilo limemaliza muda wake baada ya kupitisha miswada muhimu hasa ya bajeti, kusaidia serikali itakayoingia madarakani kuanzia mwezi Agosti.