Rwanda yatangaza kutuma wanajeshi wake nchini Msumbiji
Rwanda imeanza kutuma wanajeshi wake 1,000 nchini Msumbiji kusaidia kupambana na majihadi katika mkoa wenye utajiri wa gesi, wa Cabo Delgado.
Imechapishwa:
Hatua hii imekuja mwezi mmoja, baada ya mataifa ya Jumuiya ya kiuchumi ya Kusini mwa Afrika SADC kuamua kutumwa kwa vikosi vya kikanda kuisaidia Msumbiji.
Kwa karibu miaka minne sasa, wanajihadi wamekuwa wakipambana na wanajeshi Kaskazini mwa Msumbiji na mpaka sasa watu zaidi ya 3,000 wameuawa na wengine 800,000 wameyakimbia makwao, nusu wakiwa watoto.
Rwanda ambayo sio mwanachama wa SADC, siku ya Ijumaa, ilitangaza kutumwa kwa vikosi vyake kushirikiana na vile vya Msumbiji na vile kutoka mataifa mengine ya ukanda huo kupambana na wanajihadi hao.
Alexandre Raymakers, mchambuzi wa masuala ya Afrika kutoka Shirika la Global risk consultancy Verisk Maplecroft, anasema kikosi cha Rwanda huenda kikatumiwa kulinda maeneo muhimu yenye utajiri wa gesi, kwa lengo la kuwavutia wawekezaji wa Kimataifa.