Kundi la wakimbizi 1,000 warejea Burundi kutoka Rwanda
Wakimbizi kutoka nchini Burundi wapatao elfu moja wamerejea makwao kutoka nchini Rwanda baada ya takribani miaka 5 katika oparesheni iliyoshuhudiwa na Mkuu wa shirika la kuwahudumia wakimbizi UNHCR, Filippo Grandi.
Imechapishwa:
Kundi la kwanza la wakimbizi 159 waliondoka Jumanne wiki hii kupitia mpaka wa Ntemba.
«Nimefurahi sana, hata nyumbani walikua wakiniambia nachelewa kurejea maana hali ya usalama ni nzuri, narejea nchini kwangu. Nchi yako ni kama mzazi, unaporudi kumuona mzazi ,unakua na furaha narudi nyumbani nikiwa na furaha kwa sababu naona na wenzangu wanarejea », mmoja wa wakimbizi hao amesema.
Kurejea nyumbani kwa wakimbizi hao kumefuatia mazungumzo kati ya serikali ya Rwanda na Burundi ambapo wanarejea kwa hiyari, kulingana na Kayumba Olivier, Katibu mkuu wa wizara inayohusika na majanga na uokoaji.
Mchakato wa wakimbizi kurejea kwao unaendelea vizuri, kama ilivyoombwa na serikali ya Burundi na UNCHR ,tunasaidiana na unaendelea vizuri , wakimbizi waliofanikiwa kurejea hadi sasa ni zaidi ya elfu 21 na tukitarajia kabla ya mwisho wa mwaka huu, wakimbizi wengine wapatao elfu 20 watakua wamesharejea.
Kwa upande wake mkurugenzi wa UNHCR, Filippo Grandi, ambaye awali alikutana na rais Paul Kagame kabla ya kuelekea nchini Burundi amesema ana imani kwamba wakimbizi wote watarejea nchini mwao hivi karibuni.
Kwa sasa nchi ya Rwanda ina jumla ya wakimbizi laki moja na elfu arobaini na tisa, kati yao elfu sabini na mbili ni kutoka Burundi.