Urusi yasisitiza kuwa haina mpango wa kuivamia Ukraine
Waziri wa Mambo ya nje wa Urusi, Sergey Lavrov, amesema nchi yake haitaki vita, kauli aliyoitoa baada ya rais wa Marekani kusema kuwa Urusi inajiandaa kuivamia Ukraine, mapema mwezi Februari, huku rais Vladimir Putin akimwambia rais wa Ufaransa Emmanuel Macron kuwa nchi za Magharibi zimepuuza malalamishi yake ya kiusalama.
Imechapishwa:
Lavrov amesema, Urusi haitaki kuingia kwenye vita na Ukraine lakini, haitakubali usalama wake kutishiwa na maslahi yake ya kiusalama kupuuzwa.
Licha ya kauli hii ya Lavrov, maelfu ya wanajeshi wa Urusi kuendelea kufanya mazoezi katika mpaka wake na Ukraine kunaendelea kuzua wasiwasi kuwa, uvamizi huo huenda ukatokea.
Siku ya Ahamiisi, Marekani na muungano wa majeshi ya NATO, ulijibu masharti ya Urusi ambayo ni kutaka Ukraine isiruhusiwe kujiunga na jumuiya ya jeshi la nchi za Magharibi NATO, na kusema haiwezekani kuizua Ukraine.
Katika hatua nyingine, siku ya Ijumaa, rais wa Ufaransa Emmanuel Macron alizungumza na mwenzake wa Urusi Vladimir Putin kwa zaidi ya saa moja kuhusu mzozo huu, lakini walichokizungumza hakijawekwa wazi.
Aidha, Macron atafanya mazungumzo mengine na mwenzake wa Ukraine Volodymyr Zelensky ,wakati huu hali ya wasiwasi inapoendelea kushuhudiwa.