Burma: Aung San Suu Kyi kufikishwa mbele ya majaji
Kesi ya kiongozi aliyepinduliwa madarakani nchini Myanmar, Aung San Suu Kyi, imefunguliwa Jumatatu hii, Mei 24, wakati mvutano ukiongezeka nchini humo kati ya jeshi na wapinzani dhidi ya mapinduzi.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Makabiliano hayo yameua zaidi ya watu 800 tangu Februari 1, lakini hakuna mtu anayeweza kusema ikiwa Aung San Suu Kyi ana taarifa ya mgogoro unaoikabili nchi yake, kwani kiongozi huyo yuko chini ya kizuizi cha nyumbani tangu kukamatwa kwake.
Hii ni mara ya kwanza tangu mapinduzi ya serikali nchini Myanmar, kesi ya Aung San Suu Kyi kusikilizwa ana kwa ana. Kufikia sasa, kesi yake ilikuwa ikisikilizwa mkondoni na wakati mwingine ilisitishwa kwa sababu ya ukosefu wa mtandao, ameripoti mwandishi wetu, Juliette Verlin.
Muda mfupi kabla ya kusikilizwa, "alitaka watu wake waendelee kuwa na afya njema" na akasema kwamba chama chake, LND "kitakuwepo maadamu watu wapo, kwa sababu kilianzishwa kwa niaba ya watu. Wakili Min Min Soe ameliambia shirika la habari la AFP.
Aung San Suu Kyi akabiliwa na kifungo cha miaka mingi jela
Mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel ya 1991 ameshtakiwa mara sita tangu kukamatwa kwake. Anashtakiwa hasa kwa kukosa la kutofuata masharti yanayohusiana na janga la Corona, uingizaji haramu wa raia wa kigeni, uchochezi wa machafuko na ukiukaji wa sheria za siri za serikali za tangu enzi za ukoloni.
Pia anatuhumiwa kukusanya dola laki kadhaa na kilo kumi na moja za dhahabu kwa hongo, lakini hajashtakiwa kwa "ufisadi"
Ikiwa atapatikana na hatia, anaweza kupigwa marufuku kujihusisha na siasa, hata akahukumiwa kifungo cha miaka mingi gerezani.
Bi Suu Kyi, 75, hajaonekana hadharani tangu kukamatwa kwake nyumbani huko Naypyidaw wakati wa mapinduzi ya kijeshi.