Utafutaji wa ndege ya Indonesia Air Asia unaendelea
Waokoaji wa kimataifa bado wanaitafuta ndege ya Indonesia ya Air Asia iliyotoweka jana Jumapili Desemba 28 mwaka 2014 ikiwa na abiria 162.
Imechapishwa:
Waokoaji katika kambi ya kijeshi ya Surabaya nchini Indonesia wamesema utafutaji wa ndege hiyo unakwenda vizuri na kuna matumaini ya kupatikana.
Ndege hiyo ilipotea katika Bahari ya Java ikitokea mjini Surabaya nchini Indonesia ikielekea Singapore.
Ripoti zinasema kuwa, marubani wa ndege hiyo waliomba kubadilishiwa njia kutokana na hali mbaya ya hewa lakini hawakupiga simu ya dharura kabla ya ndege hiyo kutoweka.
Ndege maalum, pamoja na meli zinatumika kuitafuta ndege hiyo na Mataifa mbalimbali duniani yameungana kuisaidia Indonesia.
Waziri wa uchukuzi wa Indonesia, Tatang Kurniadi, amesema kazi kubwa iliyo mbele yao kwa sasa ni kuitafuta na kuipata ndege hiyo.
Miongoni mwa nchi zinazosaidia katika utafutaji wa ndege hiyo ni pamoja na Malaysia, ambayo pia ndege yake ilipotea mwaka huu katika mazingiuraya ya kutatanisha, Singapore na Australia.