Trump awatuhumu waandamanaji na vyombo vya habari kutaka kumuangusha kisiasa
Rais wa Marekani Donald Trump amezindua kampeni za kutaka kuchaguliwa tena kwa muhula wa pili huku akiwashtumu waandamanaji na vyombo vya habari kwa kujaribu kupaka tope rekodi yake ya maendeleo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Mkutano wake wa kwanza ulifanyika katika mji wa Tulsa, jimboni Oklahoma na kuhudhuriwa na watu wachache, wengi wao wakionekana bila barakoa wakati huu nchi hiyo inapoendelea kupambana na virusi vya Corona.
Trump amemshtumu mpinzani wake Joe Biden wa chama cha Demoractic katika ufunguzi wa kampeni zake.
Wakati huo huo Kikosi chake cha kampeni kimepinga madai kwamba kampeni ya mitandao ya kijamii kwa njia ya Tik-Tok na K-Pop fans ndizo zilizosababisha kujitokeza kwa idadi ndogo ya watu katika mkutano wa kampeni ya uchaguzi iliyofanyika siku ya Jumamosi usiku.
Kikosi cha zimamoto cha Tulsa kimenukuliwa kikisema kuwa zaidi ya viti 6,000 ndivyo vilivyokaliwa katika ukumbi huo, lakini kampeni ya Trump ilisema kuwa idadi ya waliohudhuria ilikua ni ya juu zaidi.
Uchaguzi nchini Marekani umepangwa kufanyika mwezi Novemba mwaka huu.