Trump atetea uamuzi wake wa kutoa siri za Islamic State kwa Urusi
Imebainika kuwa rais wa Marekani Donald Trump alitoa taarifa za siri kuhusu mipango ya kundi la kigaidi la Islamic State alipokutana na Waziri wa Mambo ya nje wa Urusi Sergei Lavrov wiki iliyopita jijini Washington DC.
Imechapishwa:
Gazeti la Washington Post limeripoti kuwa Trump alinukuliwa akimwambia Lavrov kuwa kundi la Islamic State lilikuwa linapanga kutumia kompyuta mpakato kutekeleza mashambulizi yake.
Hata hivyo mshauri wa maswala ya usalama nchini humo HR McMaste amekanusha ripoti hii ya Washington Post na kusema ni ya uongo na ya kupotosha.
Naye raisi Trump amejitokeza kupitia ukurasa wake wa Twitter na kusema kuwa ana haki ya kubadilishana taarifa muhimu na Urusi na lengo lake lilikuwa ni kuisadia katika vita dhidi ya Islamic State.
Yote haya yanajiri wakati huu wengi wakikumbuka shutuma za Trump kwa aliyekuwa mshindani wake wa karibu Hillary Clinton namna alivyoshughulikia taarifa za siri alipokuwa Waziri wa Mambo ya nje.
Imeripotiwa kuwa Trump alitoa siri hizi siku moja baada ya kumfuta kazi aliyekuwa Mkuu wa Shirika la upelelezi la FBI James Comey.