Washington yamuwekea vikwazo Meya wa Monrovia
Utawala wa Marekani umeamua kuzuia mali nchini Marekani za meya wa Monrovia, mji mkuu wa Liberia. Anashutumiwa kwa ghasia dhidi ya wapinzani wake wa kisiasa, ukiukaji wa haki za binadamu na ufisadi, unasema ubalozi wa Marekani mjini Monrovia.
Imechapishwa:
Meya, Jefferson Koijee, anatuhumiwa kuamuru makundi ya wanamgambo yenye uhusiano na chama chake, na ambayo ana udhibiti, kutenda kikatili dhidi ya maandamano ya wapinzani, wakosoaji wa serikali au wanaharakati dhidi ya ubakaji kati ya mwaka 2018 na 2022, Wizara ya Fedha ya Marekani imesema siku ya Jumamosi.
Bw. Koijee ni afisa mkuu wa CDC, chama cha rais anayemaliza muda wake George Weah ambaye alishindwa hivi majuzi katika uchaguzi wa urais na Joseph Boakai mwishoni mwa uchaguzi uliosifiwa kwa jumla kwa jinsi ulivyofanyika, katika eneo ambalo limekumbwa na mapinduzi kwa miaka kadhaa.
"Pia alijihusisha na vitendo vya rushwa, hasa kupitia hongo na ufujaji wa mali ya serikali kwa manufaa ya makundi ya kisiasa ya kibinafsi, na shinikizo kwa wachunguzi waliohusika na kupamana dhidi ya ufisadi," inaongeza Wizara ya Fedha.
Marekani imewawekea vikwazo maafisa wakuu wa Liberia katika miaka ya hivi karibuni, akiwemo aliyewahi kuwa mkuu wa majeshi ya rais Weah, kwa tuhuma za rushwa na ubadhirifu na vitendo vya vitisho dhidi ya wapinzani.
Ufisadi unachukuliwa kuwa tatizo katika nchi hii ndogo ya Afrika Magharibi, mojawapo ya nchi maskini zaidi duniani.
Sauti ya Marekani inasikika nchini Liberia kutokana na uhusiano wa kihistoria na wa sasa kati ya nchi hizo mbili na uzito wa diaspora ya Liberia upande wa pili wa Atlantiki.