Madagascar: Rais Andry Rajoelina ametangazwa mshindi wa urais
Nairobi – Tume ya uchaguzi nchini Madagascar, imemtangaza rais Andry Rajoelina kuibuka mshindi katika duru ya kwanza ya uchaguzi wa urais, zoezi ambalo hata hivyo lilisusiwa karibia na wanasiasa wote wa upinzani.
Imechapishwa:
Rajoelina ametangazwa mshindi baada ya kupata asilimia 58.95 ya kura zote zilizopigwa wakati wa uchaguzi mkuu wa tarehe 16 ya mwezi Novemba.
Tume ya uchaguzi imesema kuwa ni asilimia 46 peke ya wapiga kura walishiriki zoezi hilo, idadi hii ikionekana kuwa ndogo ikilinganishwa na namna iliyokuwa wakati wa uchaguzi wa 2018.
Rajoelina mwenye umri wa miaka 49, aliingia madarakani kwa mara ya kwanza mwaka wa 2009 baada ya mapinduzi yalioangusha utawala wa rais wa zamani Marc Ravalomanana.
Wapiga kura milioni kumi na moja kwenye taifa hilo walikuwa na kibarua cha kumchagua kati ya Rajeolina na wagombea wengine 12 wa upinzani.
Licha ya hilo, wagombea wengine 10 walikataa kushiriki uchaguzi huo na kuwataka wafuasi wao kutoshiriki zoezi hilo kwa misingi kuwa halingezingatia usawa na haki.
Rajoelina, meya wa zamani wa mji mkuu wa Antananarivo, anatuhumiwa na wapinzani wake kwa kushiriki ufisadi, kuingiwa na tamaa pamoja na kufumbia macho changamoto zinazowakabili raia.
Hadi tukichapisha taarifa hii, upinzani nchini humo haukuwa umesema iwapo utapinga ushindi huo.