Madagascar: Andry Rajoelina ashinda uchaguzi wa urais, katika duru ya kwanza
Rais anayemaliza muda wake nchini Madagascar Andry Rajoelina amechaguliwa tena kuwa mkuu wa nchi katika duru ya kwanza ya uchaguzi ambayo wagombea kumi kati ya 13 walikuwa wametoa wito wa kususia. Matokeo haya yametangazwa Jumamosi hii, Novemba 25 saa tano mchana saa za Madagascar, na Tume ya Uchaguzi. Hata hivyo matokeo haya yanapaswa kuthibitishwa na Mahakama Kuu ya Kikatiba, mahakama ya juu zaidi nchini, ndani ya siku tisa ambapo rufaa, katika tukio la mgogoro, inaweza kuwasilishwa.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu nchini Madagascar, Sarah Tétaud
Andry Rajoelina amechaguliwa tena kwa 58.95% ya kura. Ikumbukwe kwamba matokeo haya yanapaswa kuidhinishwa na Mahakama Kuu ya Katiba.
"Pamoja nami, raia wa Madagascar wamechagua njia ya mwendelezo, utulivu na amani", hivi ndivyo Andry Rajoelina ametangaza asubuhi, kupitia RFI, alipokuwa akitokea makao makuu ya Tume ya Uchaguzi (CENI).
“Nawashukuru raia wa Madagascar kwa kuonyesha ukomavu na kujieleza kwa uhuru. "Haya ni maneno yake, Andry Rajoelina.
Kiwango cha ushiriki katika uchaguzi huu kilikuwa cha chini ikilinganishwa na uchaguzi wa urais uliopita wa mwaka wa 2018. Kati ya watu milioni kumi na moja wa Madagascar waliojiandikisha kwenye orodha za uchaguzi, ni 46% tu waliopiga kura.
Mkuu huyo wa zamani wa nchi, mwenye umri wa miaka 49, alikuwa akiwania muhula wa pili kwa kiti cha urais. Hii ni mara ya pili kwake kuingia madarakani kupitia sanduku la kura. Mnamo 2009, alikuwa rais wa mpito, baada ya kuchukua mamlaka kwa nguvu.
Kwa hiyo ni ushindi mpya kwa Andry Rajoelina, ushindi ambao mgombea pekee aliushuhudia. Hakuna hata mmoja wa wagombea wengine 12, ambaye amekwenda kwenye makao makuu ya Tume ya Uchaguzi kusikiliza matokeo ya uchaguzi yalivyokuwa yakitangazwa Jumamosi hii, Novemba 25. Kumi na mmoja kati yao tayari wametangaza kwamba hawatatambua matokeo ya uchaguzi huu ambao wanaona kuwa "kinyume cha sheria na ulioguikwa na udanganyifu mkubwa".