Rwanda: Afisa wa zamani anazuiliwa kwa kuhusika kwake katika mauji ya kimbari
Nchi ya Ufaransa juma hili ilimkamata na kumfungulia mashtaka afisa wa zamani wa juu wa Rwanda, kutokana na kuhusika kwake katika mauji ya kimbari ya mwaka 1994, vyanzo katika kesi hiyo vimethibitisha.
Imechapishwa:
Pierre Kayondo, alikuwa kiongozi wa wilaya ya Kibuye na pia mbunge wa zamani, alikamatwa Jumanne ya wiki hii na kushtakiwa kwa makosa ya kuchochea mauaji na uhalifu dhidi ya binadamu.
Kayondo, alikuwa akisakwa na mamlaka za uchunguzi za Ufaransa tangu mwaka 2021, baada ya kulalamikiwa na wahanga wa vitendo vyake.
Nchi ya Ufaransa kwa miongo kadhaa imekuwa kimbilio kuu ya watuhumiwa wa mauaji ya kimbari wanaokwepa mkono wa sheria kutokana na kuhusika kwao katika mauaji ya watu zaidi ya laki 8 wengi wakiwa Watusi.
Aghalabu rais Paul Kagame, amekuwa akiinyooshea kidole Paris kwa kushindwa kuwakamata na kuwashtaki watuhumiwa wa mauaji hayo.
Uhusiaono kati ya Paris na Kigali, ulianza kurejea katika hali ya kawaida tangu kutolewa kwa ripoti ya tume iliyoundwa na rais Emmanuel Macron mwaka 2021 ambapo taifa hilo lilikiri kuzembea katika kuzuia mauaji hayo.