Marekani yaamuru kuhamishwa kwa sehemu ya wafanyakazi wake nchini Niger
Marekani imeamuru kuhamishwa kwa wafanyakazi wake wasio wa lazima katika ubalozi wa Niamey, baada ya mapinduzi ya kijeshi dhidi ya rais wa Niger Mohamed Bazoum, imetangaza Wizara ya Mambo ya Nje. Kwa upande wake, Wizara ya Mambo ya Nje ya Ufaransa ilisema siku ya Alhamisi kwamba operesheni ya kuwahamisha raia wanaotaka kuondoka Niger imekamilika.
Imechapishwa:
Operesheni ya kuwahamisha raia wanaotaka kuondoka Niger imekamilika, Wizara ya Mambo ya Nje ya Ufaransa, Quai d'Orsay, imetangaza leo Alhamisi Agosti 3 kwenye tovuti yake.
Wizara hiyo ilisema Jumatano jioni kwamba ndege ya nne iliondoka Niger kuelekea Ufaransa, na hivyo kufikisha idadi ya watu 992 waliohamishwa kutoka nchi hiyo ya Afrika Magharibi, ambapo mapinduzi ya kijeshi yalitangazwa wiki iliyopita na jeshi.
Leo Alhamisi Quai d'Orsay imelaani tena katika taarifa tofauti ghasia zilizofanywa siku ya Jumapili dhidi ya ubalozi wa Ufaransa nchini Niger, na kusema kwamba Ufaransa imevitaka vikosi vya usalama vya Niger kuchukua hatua kuhakikisha usalama kene ubalozi wa Ufaransa mjini Niamey, wakati wito ukitolewa kwa maandamano leoAlhamisi Agosti 3.
Wakati huo huo, misaada ya kimataifa kwa Niger imesitishwa, huku Benki ya Dunia ikitangaza kusitisha msaada wowote na mkopo kwa Niger.
(Pamoja na AFP)