Somalia: Raia sita na maafisa watatu wa polisi wauawa katika hoteli moja Mogadishu
Baada ya uvamizi wa Waislam wa Al-Shabab uliyodumu saa sita , mamlaka ya Somalia imepata tena udhibiti wa Pearl Beach, hoteli moja inayopatikana katika eneo maarufu la mji mkuu. Raia sita na maafisa watatu wa polisi waliuawa na raia kumi kujeruhiwa.
Imechapishwa:
Na mwanahabari wetu mjini Nairobi, Albane Thirouard
Uvamizi huo ulichukua muda wa saa sita kabla ya vikosi vya usalama kukomesha shambulio hili jipya. Jumamosi hii asubuhi Juni 10, kulionekana kwenye mitandao ya kijamii picha za hoteli ya Pearl Beach ikiwa na madirisha yaliyovunjwa na kuta zilizoharibiwa.
Shambulio hilo lilianza Ijumaa jioni, muda mfupi kabla ya saa mbili usiku, wakati washambuliaji saba walipovamia hoteli hiyo kwenye ufukwe wa Mogadishu. Mkahawa huo ulikuwa umejaa, kulingana na ushuhuda uliokusanywa na shirika la habari la AFP.
Majibizano ya kurushiana risasi kati ya wapiganaji hao wa Kiislamu na vikosi vya usalama yalifuata hadi washambuliaji walipokomeshwa, karibu saa 2 asubuhi, kulingana na polisi. Raia sita na maafisa wa polisi watatu waliuawa na raia kumi kujeruhiwa. Na "vikosi vya usalama vilifanikiwa kuokoa watu 84, wakiwemo wanawake, watoto na wazee," imesema taarifa hiyo.
Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia umelaani shambulio hilo kwenye ufukwe wa Pearl. Kwenye Twitter, umetangaza kwamba mmoja wa wafanyakazi wake, anayefanya kazi na WHO, ameuawa.
'Vita kamili'
Shambulizi hili linakuja wakati Rais wa Somalia Hassan Sheikh Mohamoud alitangaza "vita kamili" dhidi ya Al Shabab. Mnamo mwezi Septemba alianzisha mashambulizi ya kijeshi. Lakini Waislam wanaendelea kufanya mashambulizi kwa kulipiza kisasi, wakionyesha uwezo wao wa kushambulia katikati ya miji na vituo vya kijeshi.