Ntaipa Urusi silaha: Julius Malema
NAIROBI – Julius Malema, kiongozi chama cha Economic Freedom Fighters (EFF) nchini Afrika Kusini, amesema "ataipa silaha Urusi" kwa sababu Moscow iko "katika vita na ubeberu".
Imechapishwa:
Katika mahojiano na BBC mjini Johannesburg, Malema alisisitiza kwamba "Afrika Kusini ni mshirika wa Urusi" na kwamba msimamo wa serikali ya ANC wa kutojihusisha na siasa unahusu vita vya Ukraine pekee.
"Nitaenda zaidi ya urafiki na Urusi. Katika vita, nitaungana na Urusi na nitasambaza silaha,” Malema ameiambia BBC.
EFF pia kinataka Afrika Kusini kujiondoa katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC).
ICC imetoa hati ya kukamatwa kwa Vladimir Putin kwa madai ya uhalifu wa kivita lakini Bw Malema ameahidi kuzuia jaribio lolote la kumkamata rais wa Urusi iwapo atahudhuria mkutano wa kilele wa Brics mwezi ujao mjini Cape Town.
Wito wa Malema unakuja wakati huu mzozo wa kidiplomasia ambapo balozi wa Marekani nchini Afrika Kusini alidai kuwa silaha na risasi zilipakiwa kwenye meli ya Urusi iliyotia nanga nchini humo Desemba mwaka jana.
Serikali ya Afrika Kusini imekana kuidhinisha usafirishaji wowote wa silaha kwenda Urusi.