Afrika Kusini: Rais Ramaphosa aponea kutimuliwa mamlakani
Nchini Afrika Kusini, hatimaye Rais Ramaphosa ameponea kufunguliwa kwa kesi ya mashtaka Jumanne, Desemba 13. Bunge la kitaifa limepiga kura, mjini Cape Town, kuamua juu ya ripoti huru ambayo inashuku rais kwa kufanya vitendo vya kukiuka sheria.
Imechapishwa:
Cyril Ramaphosa anakabiliwa na kesi ya wizi wa angalau dola 580,000 kutoka kwa shamba lake la "Phala Phala" mnamo 2020, na anatuhumiwa kuficha wizi huo kutoka kwa mamlaka. Lakini wabunge wa chama cha ANC hatimaye waliamua kuweka imani yao kwa rais.
Wabunge 214 wamejitangaza kuunga mkono kukataliwa kwa ripoti hii ya bunge, dhidi ya 148, na 2 kujiepusha. Takriban manaibu wote wa ANC, walio wengi katika Bunge la Kitaifa, kwa hivyo walichagua kufuata mkondo wa chama na kuzuia kufunguliwa kwa kesi za kufutwa kazi.
Licha ya kura ya umma, bila kura ya siri, chaguo lililokashifiwa na wawakilishi wengi wa upinzani, maafisa 4 wa chama cha ANC 'walioasi' walionyesha kutokubaliana kwao kwa kupiga kura ya ndio, wakiongozwa na Waziri wa Mambo ya Jadi, Nkosazana Dlamini-Zuma, mpinzani mkuu wa Cyril Ramaphosa.
Wapinzani wengine wa rais Ramaphosa, mfano Zweli Mkhize anayechuana naye katika uchaguzi ujao wa ndani, au Waziri Lindiwe Sisulu, hawakuwepo katika zoezi hilo.
Kwa hivyo Rais Ramaphosa ameshinda vita na ameweza kukusanya wanajeshi wake, lakini bado atalazimika kushinda migawanyiko ili kuchaguliwa tena kuwa mkuu wa chama cha ANC wikendi hii na kurejesha imani ya Waafrika Kusini kama anataka kuongoza chama kuelekea uchaguzi mkuu wa 2024.