Afrika Kusini: Wabunge wanajadili hatma ya rais Cyril Ramaphosa
Wabunge nchini Afrika Kusini, wameanza kujadili iwapo waanzishe mchakato wa kumwondoa madarakani rais Cyril Ramaphosa kufuatia ripoti ya madai ya kuficha fedha za wizi katika makaazi yake.
Imechapishwa:
Wabunge wa upinzani wakiongozwa na Julius Malema, wameunga mkono ripoti hiyo, huku wakikishtumu chama tawala cha ANC kwa kumkingia kifua rais Ramaphosa.
Kabla ya kuanza kwa mjadala huo, wabunge walitumia muda mrefu kumshawishi spika wa bunge Nosiviwe Mapisa-Nqakula kuamua kuwa kura ya siri itumiwe kuunga mkono ripoti hiyo au la, lakini spika aliamua kuwa, kura hiyo haitakuwa ya siri.
Mjadala huu, unakuja baada ya wakuu wa chama tawala wiki iliyopita kukutana na kuamua kuwa hawatounga mkono mswada wowote utakaolenga kumwondoa madarakani rais Ramaphosa.
Kwa hali ilivyo katika bunge hilo, rais Ramaphosa ana nafasi kubwa ya kuibuka mshindi baada ya wabunge wa ANC jioni hii kuonekana kutounga mkono ripoti hiyo na kumpa nafasi ya kuwania uongozi wa nchi hiyo mwaka 2024.