Chad: Utawala watia saini kwenye makubaliano ya mazungumzo ya kitaifa na waasi
Mkuu wa utawala wa kijeshi nchini Chad, Mahamat Idriss Déby Itno, ametia saini kwenye makubaliano nchini Qatar leo Jumatatu na baadhi ya makundi arobaini ya waasi yaliyonuiwa kuzindua mazungumzo ya kitaifa tarehe 20 Agosti mjini N'Djamena, waandishi wa habari wa shirika la habari la AFP wamebainisha.
Imechapishwa:
Lakini kundi la waasi la FACT, moja ya makundi makuu ya waasi, halikutia saini kwenye makubaliano hayo, licha ya matumaini ya wapatanishi huko Doha ambao walijarubu kulishawishi hadi dakika ya mwisho.
Mpangilio huo, uliokusudiwa kufungua njia ya kurejea kwa utawala wa kiraia, uliitwa "wakati muhimu kwa raia wa Chad" na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres, ambaye amezungumza kwenye video iliyotolewa wakati wa sherehe rasmi huko Doha. Mkuu wa Umoja wa Mataifa hata hivyo alisisitiza juu ya haja ya mazungumzo "jumuishi" ili hili kufanikiwa. Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar Mohammed bin Abderrahmane al-Thani amesema makubaliano hayo yanalenga kuleta "amani ambayo itachukua nafasi ya machafuko na mzozo ambao nchi hiyo imekumbwa kwa miaka mingi." Baadhi ya makundi 42 kati ya 47 yaliyowakilishwa mjini Doha yalitia saini zao leo Jumatatu, sambamba na mamlaka.
Kwa muda wa miezi mitano, wadau mbalimbali kutoka Chad wamekuwa wakijadiliana chini ya mwamuli wa Qatar ili kukomesha miongo kadhaa ya machafuko na ukosefu wa utulivu katika nchi hii yenye wakazi milioni 16 ambayo imekumbwa na mapinduzi kadhaa. Siku moja baada ya kifo cha Rais Idriss Déby Itno, aliyeuawa na waasi akiwa vitani mwezi Aprili 2021, mtoto wake wa kiume, jenerali Mahamat Idriss Déby Itno, alitangazwa kuwa rais akiongoza Baraza la Mpito la Kijeshi la majenerali 15. Mara moja aliahidi uchaguzi huru na wa kidemokrasia ndani ya miezi 18, baada ya "mazungumzo jumuishi ya kitaifa" na upinzani wa kisiasa na makundi mengi ya waasi.