Madagascar: Madarasa 2,600 yaharibiwa na Kimbunga Batsirai
Madagascar imeendelea kukumbwa na majanga mbalimbali ikiwa ni pamoja na Covid-19, Kimbunga Ana na mafuriko yake mabaya, kimbunga Batsirai, dhoruba Dumako… Shule zimeathirika pakubwa kwa majanga haya mfululizo.
Imechapishwa:
Wanafunzi 134,000 bado hawajaweza kurejea shuleni kutokana na uharibifu wa miundombinu ya shule, lakini pia madarasa yatumika kwa sasa kama sehemu za hifadhi kwa watu waliokosa makazi yao. Wanafunzi hao ni pamoja na wanafunzi wanaoishi katika maeneo yaliyoathiriwa zaidi na kimbunga, kama vile Mananjary.
Shule ya msingi ya umma (EPP) Manara-penitra katika wilaya iliyoharibiwa ya Fangato, ilizinduliwa mwezi Oktoba mwaka uliyopita na Rais wa Jamhuri. Sehemu ya paa yake ilisombwa na kimbunga, hata kabla ya wanafunzi kuanza shule. Madarasa ambayo hayakuathirika zaidi yanatumika kama sehemu za hifadhi kwa familia zilizoathiriwa.
Katika kisiwa hicho, madarasa 2600 yaliharibiwa kabisa na 2000 hata kama yameharibiwa yanaweza kukarabatiwa. shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF lina mpango wa kuzipatia shule 500 vifaa vya shule na kusaidia baadhi ya shule zilizoathirika kwa kuzinunulia mabati. Huko Mananjary, ambapo asilimia 90 ya majengo yaliharibiwa, wanajeshi, wakaazi na karibu waokoaji thelathini wa Ufaransa walianza jana kusafisha majengo matatu ya shule ya jiji hilo kwa nia ya kukarabati.