Kimbunga Batsirai chaua watu 20 na kuharibu mashamba ya mpunga nchini Madagascar
Nchini Madagascar, kimbunga Batsirai kimesababisha vifo vya watu 20 na kusababisha wengine zaidi ya Elfu 55 kusalia bila makaazi wakati huu Umoja wa Mataifa ukionya kuhusu hali mbaya ya hali ya kibinadamu katika kisiwa hicho.
Imechapishwa:
Kimbunga Batsirai kiliondoka Madagascar Jumatatu asubuhi bila kuathiri miji mikuu, baada ya kuua watu 20 kulingana na ripoti ya hivi punde kutoka kwa mamlaka.
Hata hivyo mafuriko yameharibu "mashamba ya mchele" katikati mwa kisiwa hicho, na kuzua hofu ya kuzorota kwa hali ya kibinadamu, UNICEF imeonya.
"Kimbunga Batsirai ameondoka Madagascar leo saa moja asubuhi kwenda Ghuba ya Msumbiji," Jean Benoit Manhes, naibu mwakilishi wa UNICEF nchini Madagascar, ameliambia shirika la habari la AFP. Kulingana na ripoti ya hivi punde kutoka Ofisi ya Kudhibiti Hatari na Majanga (BNGRC), watu 20 wameuawa na 55,000 walilazimika kutoroka makazi yao.
Kimbunga hicho cha kitropiki kilitua usiku wa Jumamosi kuamkia Jumapili kwenye pwani ya mashariki ya kisiwa hicho kikubwa katika Bahari ya Hindi na mvua kubwa na upepo mkali uliotembea hadi kilomita 165 kwa saa, baada ya kupiga kisiwa cha Ufaransa cha Réunion. Unicef inahofia kwamba waathiriwa wengi ni watoto, katika nchi ambayo wanawakilisha zaidi ya 50% ya raia.
Kimbunga hicho kilipiga kwa mara ya kwanza eneo la pwani lenye urefu wa kilomita 150 lenye watu wachache na la kilimo. Kabla ya kuelekea magharibi mwa nchi kavu, na kusababisha mafuriko ya mito ambayo yaliharibu mashamba ya mpunga katikati mwa nchi, kulingana na UNICEF.
“Madhara ya kimbunga hicho hayaishi leo, yatadumu kwa miezi kadhaa hasa katika sekta ya kilimo,” ameonya Bw.Manhes. Moja ya nchi maskini zaidi duniani, Madagascar ilikuwa tayari imekumbwa na dhoruba mbaya ya kitropiki, Ana, ambayo iliua watu 55 katika kisiwa hicho na makumi ya maelfu ya watu waliopoteza makaazi yao.