Chad: Albert Pahimi Padacké ateuliwa kuwa Waziri Mkuu
Albert Pahimi Padacké ameteuliwa kuwa Waziri Mkuu, kiongozi wa serikali ya mpito, kwa agizo la rais lililosomwa kwenye redio ya serikali na msemaji wa Baraza la Kijeshi l Mpito (CMT).
Imechapishwa:
Uteuzi huu uliofanyika leo Jumatatu Aprili 2, unakuja karibu wiki moja baada ya kuundwa kwa baraza la kijeshi la mpito linaloongozwa na Mahamat Idriss Déby, mtoto wa hayati rais Idriss deby Itno.
Albert Pahimi Padacké alikuwa Waziri Mkuu wa Rais Déby kutoka mwaka 2016 hadi 2018. Kiongozi huyo wa chama cha kisiasa cha RNDT-Le Réveil, alichukuwa nafasi ya pili kulingana na matokeo ya muda ya uchaguzi wa rais wa Aprili 11, 2021.
Jeshi lafutilia mbali mazungumzo na waasi
Hayo yanajiri wakati Baraza Kijeshi la Mpito limekataa ombi la mazungumzo ya kusitisha vita na waasi ambao imekuwa ikipigana nao tangu kifo ambacho hakikutarajiwa cha rais Idris Deby.
Viongozi wa upinzani na waasi wameshutumu hatua ya jeshi kuchukua madaraka kama mapinduzi.
Idriss Deby aliyekuwa na umri wa miaka 68 alikuwa ameshinda uchaguzi wa urais wakati jeshi lilipotangaza siku ya Jumapili kwamba aliuawa katika vita dhidi ya waasi katika eneo la kaskazini mwa jimbo la Kanem katika taifa hilo la katikati mwa Afrika.
Waasi hao wanaojulikana kwa jina Front for Change and Concord in Chad (FACT),walifagia eneo la kaskazini siku ya uchaguzi wakitaka bwana Deby kusitisha uongozi wake wa miaka 30.