Chad: Makabiliano yazuka kati ya jeshi na waasi wa FACT katika mkoa wa Kanem
Makabiliano ya kwanza kati ya vikosi vya serikali na waasi wa Front for Alternation and Concord in Chad (FACT), yalizuka kaskazini mwa mji wa Mao, katika mkoa wa Kanem.
Imechapishwa:
Msururu wa waasi hao , waliovuka mpaka na kuingia kwenye ardhi ya Chad kutoka Libya Aprili 11, waliingia tena katika eneo hili lililoko chini ya kilomita 300 kutoka mji mkuu kabla ya kukabiliana na vikosi vya serikali.
Mapigano hayo yalifanyika karibu saa 9:30 alaasiri siku ya Jumamosi kaskazini mwa Kanem. Waasi, walioripotiwa siku mbili zilizopita huko Gouri, kilomita 200 kaskazini mwa mji wa Faya Largeau, mji mkuu kaskazini mwa Chad, walitoweka kutoka kwenye rada na ikuoneana tena katika eneo la kusini siku ya Jumamosi.
Waasi waapa kuendelea na mapigano
Jeshi, lililopewa taarifa kutoka kikosi cha wanaanga, lilikuwa likisubiri waasi katika eneo hili lenye matuta ya mchanga. Kwa sasa hakuna idadi ya watu waliouawa au kujeruhiwa katika mapigano hayo ingawa jeshi linasema limewashinda wale linalowaita "magaidi".
Kulingana na vyanzo kadhaa vya usalama, waasi wamegawanyika katika makundi kadhaa kushambulia pande kadhaa, hali ambayo inawafanya waseme kwamba mapigano ya Jumamosi hayawezi kuwa ya mwisho.
Hali inayotia wasiwasi serikali ya Ndjamena ambapo baadhi ya watu wameanza kuweka vyakula vya akiba kwenye ghala zote. Na kwenye wavuti ya ubalozi wa Ufaransa nchini Chad, kumechapishwa habari inayowashauri raia kuepuka kutoka mji mkuu.