Raia wa Chad wasubiri matokeo ya uchaguzi
Kura zinaendelea kuhesabiwa nchini Chad, baada ya wananchi kupiga kura kumachagua rais wakati huu kiongozi wa muda mrefu Idris Deby Itno akitarajiwa kushinda tena.
Imechapishwa:
Siku moja baada ya raia kushiriki Uchaguzi Mkuu siku ya Jumapili, Tume ya uchaguzi nchini, imeanza kuhesabu kura na ina hadi tarehe 25 kumtangaza mshindi wa uchaguzi huu.
Rais Idriss Deby Itno ambaye ametawala nchi hiyo kwa miaka thelathini amewania urais kwa muhula wa sita, licha ya upinzani nchini humo kutangaza kususia uchaguzi huo.
Viongozi wa upinzani walijiondoa kwenye kinyang'anyiro hicho wakilalamikia kunyanyaswa na maafisa wa usalama na baada ya jaribio la kukamatwa mgombea wa upinzani Yaya Dillo mwezi wa Februari, na sasa wameapa kuzua fujo iwapo rais Deby atatangazwa mshindi.
Wagombea wengine sita wanaopambania nafasi hiyo ni pamoja na aliyekuwa waziri mkuu wa nchi hiyo Albert Pahimi Padacke na aliyekuwa waziri wa kilimo Lydie Beasemda ambaye anakuwa mwanamke wa kwanza kuwania nafasi hiyo nchini Chad.