Chad yajiandaa kwa uchaguzi wa Jumapili
Tume ya uchaguzi nchini Chad inasema kuwa maandalizi yote yamekamilika, kuelekea uchaguzi wa urais utakaofanyika siku ya Jumapili Aprili 11.
Imechapishwa:
Rais wa muda mrefu Idriss Derby Itno ambaye amekuwa madarakani kwa zaidi ya miaka 30, anatarajiwa kurejea tena madarakani.
Hivi karibuni kiongozi wa chama cha upinzani cha Transformateurs nchini Chad alitoa wito wa kususiwa uchaguzi mkuu ujao wa Aprili 11 akiutaja kuwa ni wa kimaonyesho tu.
Dkt Succès Masra ambaye alikuwa akihutubia waandishi wa habari katika makao makuu ya chama hicho mjini N'Djamena aliituhumu serikali ya rais Idriss Deby kuwa inanyanyasa wapinzani na kuwaonyesha waandishi habari mabaki ya risasi ambazo amesema zilifyatuliwa na polisi kwenye mkutano wa kisiasa wa vyama vya upinzani.
Masra amesema zoezi lililopangwa kufanyika tarehe 11 ni utani na mchezo na kwa msingi huo kambi ya upinzani inafanya kila liwezekanalo kuhakikisha kwamba uchaguzi huo unasusiwa na wananchi.