Mvutano kati ya Rwanda na Uganda: Uganda yatoa wito kwa raia wake kuwa watulivu
Waziri Mkuu wa Uganda Ruhakana Rugunda, ametoa wito wa utulivu kipindi hiki nchi yake na Rwanda ikiendelea kuvutana kuhusu kufungwa kwa mpaka wa Katuna.
Imechapishwa:
Rwanda ilieleza hatua hiyo ni kwa sababu ya ukarabati wa mpaka huo lakini Uganda inasema, nchi hiyo ya jirani ilikwenda kinyume na taratibu za Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Rugunda amesema, nchi yake na Rwanda ni ndugu na mataifa jirani na juhudi zinafanyika kutatua mvutano uliopo.
Siku ya Ijumaa serikali ya Uganda ilimtaka Balozi wa nchi ya Rwanda nchini humo Meja Jenerali Frank Mugambage kueleza mvutano wa kidiplomasia kuhusu sintofahamu kati ya mpaka wa nchi hizo jirani.
Hivi karibuni, Waziri wa Mambo ya nje wa Rwanda Richard Sezibera alinukuliwa akisema raia wa nchi yake wanateswa nchini Uganda, madai ambayo serikali ya Uganda imekanusha.
Serikali ya Rwanda, imewataka raia wake wanaokwenda nchini Uganda kuwa makini, kwa madai kuwa raia wake wanakamatwa na kurudishwa nyumbani kwa nguvu.