UN: Watu zaidi ya 280 wameuawa tangu mwanzoni mwa mwaka 2018 Mali
Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa imesema mamia ya raia wameuawa nchini Mali mwaka huu pekee, katika makabiliano baina ya makundi hasimu ya waasi.
Imechapishwa:
Rupert Colville, msemaji wa ofisi hiyo amesema kwa ukali, “raia 289 wameuawa katika matukio 99 ya mapigano baina ya makundi hasimu ya waasi au vita vya kikabila tangu mwanzoni mwa mwaka huu hadi sasa.”
Amesema hayo ni kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na kikosi cha Kulinda Amani cha Umoja wa Mataifa (MINUSMA); na kwamba asilimia 75 ya visa hivyo vimetokea katika eneo la Mopti, katikati mwa nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika.
Kwa mujibu wa uchunguzi huo wa MINUSMA, chanzo cha mapigano hayo ya kikabila huanzishwa na waasi wa kabila la Dozo (wawindaji wa asili), dhidi ya vijiji vya watu wa jamii ya Fulani.
Nchi ya Mali ilikumbwa na ghasia na ukosefu wa amani baada ya mapinduzi yaliyotokea nchini humo mwaka 2012.