Kesi ya mwandishi wa RFI Ahmed Abba kusikilizwa Alhamisi hii Cameroon
Kesi ya muandishi wa habari wa RFI idhaa ya Hausa nchini Cameroun, Ahmed Abba inatarajiwa kusikilizwa Alhamisi hii katika mahakama ya rufaa jijini Yaunde, nchini Cameroon.
Imechapishwa:
Ni miaka miwili sasa tangu kutiwa nguvuni kwa mwandishi huyo wa habari kwa tuhuma za ugaidi, ambapo katika hatua ya kwanza alisafishwa na tuhuma hizo na baadae kutuhumiwa kosa la kutotoa taarifa kuhusu ugaidi.
Mawakili wa Muhamed Abbas wanasema kuna matumaini ya mteja kushinda kesi hiyo.
Hayo yanajiri wakati ambapo Shirika linalotetea Waandishi wa Habari (CPJ) lilitoa ripoti inayoshtumu serikali ya Cameroon kuminya uhuru wa vyombo vya habari nchini humo.
Ripoti hii inaonyesha tena jinsi sheria ya kupambana na ugaidi ya mwaka 2014 inavyotumiwa kuminya vyombo vya habari au upinzani. Katika suala hili, kesi ya mwandishi wa Idhaa ya Hausa ya RFI, Ahmed Abba, anayezuiliwa jela miaka miwili sasa, ni ushahidi tosha, amesema Robert Mahoney, naibu mkurugenzi wa CPJ.
Waziri wa Mawasiliano na msemaji wa serikali ya Cameroon amejibu kuhusu ripoti ya shirika linalotetea Waandishi wa Habari (CPJ) juu ya uhuru wa vyombo vya habari nchini humo.
Issa Tchiroma-Bakary amefutilia mbali mashtaka dhidi ya serikali yake kuwa inaminya uhuru wa vyombo vya habari, huku akihakikisha kuwa nchi yake inaheshimu uhuru wa vyombo vya habari, lakini amekumbusha kwamba Cameroon iko katika vita.