Raia wa Angola wapiga kura huku rais Dos Santos akistaafu
Raia wa Angola wanapiga kura katika Uchaguzi wa kihistoria, unaomaliza uongozi wa rais Jose Eduardo Dos Santos aliyeongoza nchi hiyo kwa miaka 38.
Imechapishwa:
Wapiga kura Milioni 9 wanashiriki katika zoezi hilo katika Uchaguzi ambao wachambuzi wa siasa wanasema mgombea wa chama tawala cha MPLA anatarajiwa kuibuka mshindi.
Waziri wa Ulinzi Joao Lourenco aliteuliwa kuwa mrithi wa rais Santos katika Uchaguzi huu, na uhusiano wake wa karibu na kiongozi huyu anayestaafu kumpa nafasi kubwa ya kushinda Uchaguzi huo.
Chama cha MPLA, kimekuwa kikiongoza nchi hiyo tangu ilipopata uhuru kutoka kwa Ureno mwaka 1975.
Hata hivyo, Lourenco anakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa mgombea wa chama cha UNITA Isaias Samakuva, ambaye ameahidi mabadiliko nchini humo.
Zoezi la upigaji kura litamalizika baadaye leo jioni na hesabu ya kura kuanza.