Madaktari Mashariki mwa DRC wagoma kulalamikia utovu wa usalama
Madaktari katika jimbo la Kivu Kaskazini Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, wanagoma kuishinikiza serikali kuimarisha usalama nchini humo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Kiongozi wa Madaktari hao Barie Katembo amesema wana haki ya kuwa na mgomo kuhakikisha kuwa usalama unarejea katika eneo hilo na kuikumbusha serikali jukumu lake la kupambana na makundi ya waasi.
“Watu kuwa na afya nzuri na usalama hiyo ni kazi ya serikali ,” amesema Katembo.
“Hakuna Daktari anayeweza kufanya kazi vizuri katika mazingira yenye vita, hatutaki kuendelea kuuawa kila wakati,” ameongeza.
Mgomo huu unakuja baada ya mauaji ya Daktari mwenzao Deo Chiza mwishoni mwa mwezi uliopita, hali ambayo imezua hali ya wasiwasi katika sekta ya afya nchini humo.
Chiza aliuawa katika mji wa Masisi baada ya kuvamiwa na waasi wa Mai-Mai Nyatura.
Haijabainika ni lini mgomo huu utamalizika huku hofu ikiwa ni kwa raia ambao watakosa huduma za afya na kuhatarisha maisha yao.
Makundi mbalimbali ya waasi yameendelea kusababisha hali ya wasiwasi kwa kipindi kirefu Mashariki mwa nchi hiyo na kusababisha vifo vya maelfu ya watu, huku wengine wakiyakimbia makwao.
Serikali katika jimbo hilo limetoa wito kwa Madaktari hao kuachana na mgomo huo, huku ikiendelea kuahidi kupambana na makundi ya waasi.