Congo: hali yarejea kuwa shwari Brazzaville baada ya ghasia Jumanne
Hali ya usalama katika mji mkuu wa Congo, Brazzaville, imerejea kuwa tulivu baada ya kukamatwa kwa viongozi kadhaa wa upinzani na kushuhudiwa kwa mapigano zaidi kati ya vikosi vya usalama na waandamanaji wanaopinga kufanyika kwa kura ya maoni Jumapili juma hili.
Imechapishwa:
Iwapo kura hiyo itapigwa itakua ni fursa kubwa kwa Rais Denis Sassou Nguesso kuwania urais kwa muhula mwingine baada ya kuongoza kwa zaidi ya miaka 30.
Duru za serikali zimearifu kwamba hadi sasa watu wanne ndio waliopoteza maisha katika ghasia zilizoanza siku ya Jumanne katika mji mkuu Brazzaville na Pointe-Noire, mji mkuu wa kiuchumi.
Hata hivyo wanaharakati wanasema idadi ya waliopoteza maisha inawezakuwa kubwa zaidi ya hiyo inayotolewa na serikali.
Akizungumzia hali inayojiri kwa sasa nchini Congo Brazaville, Rais wa ufaransa François Hollande amesema ni haki kwa Rais Sassou kujadiliana na wananchi wake.
Kauli hii ya Rais Hollande imewaghadhabisha wanaharakati wa mashrika ya kiraia nchini Congo.
Kura hiyo ya maoni imepangwa kufanyika Jumapili Juma hii, na iwapo kura ya ndio itashinda, basi itampa nafasi rais Sassou kuwania tena urais.