UN yalaani uamzi wa serikali ya Juba
Umoja wa Mataifa umelaani hatua ya serikali ya Sudan Kusini kumfukuza nchini humo mwakilishi wake anayeshughulikia maswala ya kibinadamu, Toby Lanzer.
Imechapishwa:
Katibu Mkuu wa Umoja huo Ban Ki Moon ameitaka serikali ya Juba kubadilisha uamuzi huo haraka iwezekanavyo ili raia wanaokimbia kutokana na machafuko waendelea kupata msaada wake.
Bwana Lanzer, raia wa Uingereza amesema hakupewa sababu yoyote ya kutakiwa kuondoka nchini humo.
Hata hivyo, muda wa kuhudumu kwa Lanzer ulikuwa unafikia ukingoni na nafasi hiyo itachukuliwa na Eugene Owusu kutoka Ghana.
Wakati huo huo viongozi wa Afrika Mashariki wamerejelea tena jitihada za kuwapatanisha viongozi wa Sudan Kusini, rais Salva Kiir na kiongozi wa waasi Riek Machar ili kumaliza mzozo unaondelea.
Ujumbe wa wawakilishi kutoka mataifa hayo pamoja na wanasiasa wa upinzani watano akiwemo katibu mkuu wa chama cha SPLM, Pagan Amum, waliokamatwa na kuachiliwa huru na serikali ya Juba na kwenda kuishi nchini Kenya walirudi nyumbani Jumatatu wiki hii.
Makamu wa rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa ndiye aliongoza ujumbe wa kuwarejesha wanasiasa hao nyumbani.