Pata taarifa kuu
LIGI YA MABINGWA-SHIRIKISHO AFRIKA-SOKA

CAF: Fahamu miamba iliyofuzu hatua ya inayofuata ligi ya mabingwa na shirikisho Afrika

Michuano ya kombe la ligi ya mabingwa barani Afrika na ile ya kombe la shirikisho imeendelea mwishoni mwa juma ambapo timu kadhaa zimefanikiwa kufuzu kucheza hatua ya makundi huku nyingine zikisubiri michezo zaidi kufuzu hatua hiyo.

Wachezaji wa Wydad wakishangilia baada ya kuwa mabingwa wa kombe la Super Cup mwaka 2018.
Wachezaji wa Wydad wakishangilia baada ya kuwa mabingwa wa kombe la Super Cup mwaka 2018. Cafonline.com
Matangazo ya kibiashara

Kwenye michuano ya ligi ya mabingwa klabu ya Plateau United ya Nigeria ikiwa nyumbani ilifanikiwa kutinga hatua ya makundi baada ya kuilaza klabu ya Etoile sahel ya Tunisia kwa bao 1-0.

AS Vita Club ya DRC ikiwa nyumbani ililazimishwa sare ya mabao 2-2 dhidi ya klabu ya Difaa El Jadidi ya Morocco, ambapo El Jadidi imetinga hatua ya makundi kutokana na faida ya bao la nyumbani ambapo mchezo wa awali ilishinda kwa bao 1-0.

Esperance Tunis ya Tunisia yenyewe imesonga mbele kuingia hatua ya makundi baada ya kuchomoza na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya mabingwa wa ligi kuu ya Kenya Gor Mahiya.

ASEC Mimosas ya Ivory Coast yenyewe ilitupwa nje kwenye hatua hii na klabu ya ZESCO ya Zambia baada ya kukubali kipigo cha mabao 2-1 na hivyo ZESCO kutinga hatua ya makundi.

Mamelodi Sundwons ya Afrika Kusini yenyewe imefuzu hatua ya makundi ya ligi ya mabingwa baada ya kuchomoza na ushindi dhidi ya Rayon Sport ya Rwanda baada ya kuchomoza na ushindi wa mabao 2-0.

Timu nyingine zilizofuzu hatua ya makundi kutokana na mechi za Jumapili ni pamoja na Al-Hilal Omdurman ya Sudan na ES Setif ya Algeria.

Kwenye kombe la shirikisho klabu ya Fosa Juniors ya Madagascar ilifuzu hatua inayofuata kwa kuchomoza na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Port Louis ya Mauritius, wakati ben Guerdane ya Tunisia ikifuzu kwa ushindi ya mabao 3-1 dhidi ya CAR Brazaville ya Congo.

Costa do Sol ya Msumbiji yenyewe ilisonga mbele baada ya kuifunga Cape Town City ya Afrika Kusini kwa mabao 2-1, huku Akwa United ya Nigeria yenyewe ikisonga mbele kwa kuifunga Al-Ittihad ya Libya.

Deportivo Niefang yenyewe ilisonga kwa kuifunga Motema Pembe ya DRC kwa bao 1-0 huku Enyimba ya Nigeria yenyewe ikichomoza na ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Energie Sports ya Benin na kusonga mbele.

Timu nyingine zilizofuzu ni pamoja na Welayta Dicha ya Ethiopia iliyowaduwaza Zamaleck ya Misri na AS Maniema ya DRC.

Hata hivyo timu zilizosonga mbele kwenye kombe la shirikisho sasa zitalazimika kucheza na timu zilizotolewa kwenye kombe la ligi ya mabingwa ili kupata timu zitakazofuzu kwenye hatua ya makundi ya kombe hilo.

Kusambaza :
Ukurasa haipatikani

Maudhui unayojaribu kuyatafuta hayapatikani kwa sasa au yamekwishaondolewa.