Uchaguzi wa urais Urusi: Mwanamke ateketeza kwa moto kibanda cha kupigia kura Moscow
Mwanamke amechoma moto kibanda cha kupigia kura katika kituo cha kupigia kura cha Moscow leo Ijumaa Machi 15, 2024, siku ya kwanza ya uchaguzi wa urais nchini Urusi, limeripoti shirika la habari la serikali la Ria Novosti, wakati hatua zinazolenga kuvuruga uchaguzi zinaongezeka nchini Urusi.
Imechapishwa:
"Tume ya uchaguzi ya Moscow imeliambia shirika la habari la Ria Novosti kwamba shughuli (katika kituo cha kupigia kura) zimeanza tena kama kawaida baada ya tukio hilo," kulingana na shirika hilo. Video iliyorushwa na vyombo huru vya habari SOTAVision inaonyesha kukamatwa kwa mshukiwa baada ya moto kuzimwa katika kituo cha kupigia kura.
Wapiga kura kwa siku tatu kuanzia leo, wanashiriki kwenye uchaguzi wa urais, unaotarajiwa kumpa Vladimir Putin nafasi nyingine ya kuongoza taifa hilo kwa miaka sita zaidi.
Uchaguzi huu unafanyika wakati huu Urusi ikiwa kwenye vita na jirani yake Ukraine kwa mwaka wa tatu sasa.
Kuanzia leo mpaka Jumapili, mamilioni ya wapiga kura wanatarajiwa kupiga kura, ambapo Putin mwenye umri wa miaka 71, anakabiliwa na wagombea wengine watatu.
Hata hivyo, wachambuzi wa siasa za Urusi wanasema itakuwa ni vigumu kumshinda Putin, ambaye ambaye amehakikisha kuwa wagombe wake wakuu wamefungwa jela au kukimbia nchi.
Mpinzani wake mkuu Alexei Navalny, alipoteza maisha hivi karibuni akiwa gerezani.
Aidha, wachambuzi wanasema hakuna matumaini kuwa uchaguzi huo utakuwa huru na haki na rais Putin anatarajiwa kupata ushindi mkubwa.