Urusi yarusha makombora usiku kucha katika miji kadhaa nchini Ukraine
NAIROBI – Nchini Ukraine, watu wawili wameuawa na wengine wamejeruhiwa baada Urusi kurusha makombora katika miji kadhaa ya nchi hiyo usiku wa kuamkia leo, likiwemo jiji kuu Kyiv.
Imechapishwa:
Meya wa mji wa Dnipro, Borys Filatov, amesema mwanamke mmoja na mtoto wa miaka mitatu, wameuawa leo asubuhi baada ya maakazi yao kushambuliwa.
Imekuwa mara ya kwanza kwa jiji la Kiev kushuhudia mashambulio baada ya zaidi ya siku 50 huku taarifa za kijeshi zikisema, makombora 11 na ndege mbili zisozokuwa na rubani, zimeangushwa.
Aidha, ripoti zaidi zinaeleza kuwa mapigano makali yanaendelea katika jimbo la Donbasa hasa mjini Bakhmut.
Mashambulio hayo pia yanakuja baada ya mawasiliano ya simu ya kihistoria kati ya rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy na rais wa China Xi Jinping, ya kwanza kati ya viongozi hao wawili tangu Moscow ilipoanza uvamizi wake kamili Februari 2022.
"China daima inasimama upande wa amani na msimamo mkuu wa China ni kukuza amani kupitia mazungumzo," gazeti la serikali la Global Times lilimnukuu Xi akisema wakati wa mawasiliao ya simu kati ya viongozi hao wawili.
China ilizindua mpango wake wa amani wenye pointi 12 kuhusu Ukraine - ikitoa wito wa kupunguzwa kasi na hatimaye kusitishwa kwa mapigano - katika kumbukumbu ya mwaka wa kwanza wa uvamizi kamili wa Urusi.