Uingereza : Mawaziri wa afya na fedha wajiuzulu
Mawaziri wawili wamejiuzulu nchini Uingereza katika hatua inayoonekana kuyumbisha uongozi wa waziri mkuu Boris Johnson.
Imechapishwa:
Waliojiuzulu ni Waziri wa afya Sajid Javid na mwenzake wa fedha Rishi Sunak, kwa kile wanachosema hawana imani na Waziri Mkuu Boris baada ya kuomba radhi kwa kile alichokieleza kuwa hakufahamu kuwa mmoja wa wafanyakazi wa serikali, ambaye pia ni Waziri wa zamani, alihusika na utovu wa nidhamu wa kingono.
Wawili hao wamesema hawawezi kuvumilia tena utamaduni wa kashfa ambazo kwa miezi kadhaa sasa umemkumba Waziri Mkuu Boris Johnson.
Boris ambaye ameonekana kujaribu kudhibiti mpasuko katika serikali yake, amemteua Waziri wa zamani wa elimu Nadhim Zahawi kuwa Waziri mpya wa fedha, huku Steve Barclay akiteuliwa kuwa Waziri mpya wa afya.
Leo, Johnson, atakuwa na kibarua kigumu bungeni, ambapo kwanza atahudhuria kikao cha kila wiki cha maswali kwa Waziri Mkuu ambako anatarajiwa kupata shinikizo za kujiuzulu.
Mwezi uliopita, Waziri Mkuu huyo alishinda kura ya kuwa na imani naye ilifanywa na chama chake cha Conservative.